Monday, July 2, 2012

Uzalendo wawakimbiza Wataalamu Zanzibar

Habari zote na Juma Mohammed, MAELEZO Zanzibar
Kukosekana kwa uzalendo na tama ya kipato kikubwa kumetajwa kuwa sababu ya ya baadhi ya wananchi wataalam kuacha kazi Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na kukimbilia ughaibuni.
Akijibu swali katika Baraza la Wawakilishi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Haji Omar Kheri alikiri kuwepo kwa tatizo la wataalam wa kizalendo kuondoka nchini kwa kutafuta maslahi zaidi nje ya nchi.
 Katika swali la msingi,.  Mwakilishi wa Jimbo la Wawi (CUF) Saleh Nassor Juma alitaka kujua sababu za wataalamu kuendelea kukimbia nchini.
Mwakilishi huyo apamoja na Mwakilishi wa Salum Abdallah Hamad (CUF) wa Matambwe, Rashid Seif Suleiman (CUF) wa Ziwani na Jaku Hashim Ayoub wa Jimbo la Muyuni (CCM) wote walilalamika kuwa serikali inachangia kuwatorosha wataalamu kwa kuwawekea mazingira mabaya ya utendaji kazi na malipo duni.
“Naomba nikubaliane na wajumbe wa baraza la wawakilishi kuwa nchi nyingi zilizopo kwa janga la sahara hukimbiwa sana na wataalamu wake hususan madaktari wakiwemo pia maprofesa na wahadhiri licha ya kulipwa stahiki mbali mbali” alisema waziri Kheri.
Waziri alisema Zanzibar pia imekuwa ikikabiliwa na tatizo la kukimbiwa na wataalamu wake hasa kada ya udaktari hospitali ambao wanakwenda nchi nyengine kupata maslahi mazuri zaidi.
Hata hivyo waziri huyo alisema miongoni mwa sababu zinazosababisha wataalamu kukimbia ni ukosefu wa maslahi bora na vitendea kazi lakini kubwa zaidi ni kukosa uzalendo.
“Serikali imekuwa ikifanya juhudi za kuimarisha maslahi ya watumishi wake na kuanzia mwaka jana wataalamu mbali mbali walirekebishiwa mishahara pamoja na posho wakiwemo madaktari lakini licha ya hilo kutokana na kukosekana uzalendo baadhi ya madaktari wanaondoka” alilalamika waziri huyo.
Waziri Kheri aliwataka wajumbe wa baraza la wawakilishi kusaidia katika juhudi za kuwashawishi wataalamu waliokuwepo nchini kupenda nchi yao na kuwatumikia wananchi huku serikali ikifanya juhudi za kuimarisha maslahi na mazingira bora ya kazi.

0 comments: