Thursday, July 5, 2012

WAKAZI 8000 WAFAIDIKA NA HUDUMA ZA BENKI YA DUNIA, MKOA WA RUKWA


Diwani kata ya MWIMBI wilaya MPYA ya KALAMBO Mkoa wa Rukwa Leonard Shalamwana (wa tatu kulia)akimuonesha Mkuu wa wilaya Moshi Mussa Chang'a(wa tatu kushoto) chanzo cha Mradi wa maji utakaogharimu zaidi ya shilingi milioni 158.3 na kunufaisha takribani wakazi 8,000. Mradi huo unadhaminiwa na benki ya dunia, wananchi pamoja na mfuko wa maendeleo wa jimbo la Kalambo. Wengine kutoka kushoto ni Mratibu wa Miradi ya TASAF wilaya John Kiondo na Kaimu Mkurugenzi wilaya Sumbawanga Crispin Luanda. 
NA RAMADHANI JUMA,
AFISA HABARI, SUMBAWANGA
WAKAZI wapatao 8,000 wa vijiji viwili vya Majengo na Mwimbi katika Kata ya Mwimbi wilaya mpya ya Kalambo Mkoa wa Rukwa wanatarajia kunufaika na mradi wa maji safi unatekelezwa katika kata hiyo kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 158.3.
Mradi huo unadhaminiwa na Benki ya Dunia iliyotoa zaidi ya shilingi milioni 154.4, wakazi wa kata hiyo wamechangia shilingi 2,709,000 na mfuko wa jimbo la Kalambo umetoa shilingi 1,200,000 ili kufanikisha mradi huo.
Akielezea mradi huo mbele ya Mkuu wa wilaya ya Kalambo Moshi Mussa Chang’a, diwani wa Kata ya Mwimbi Leonard Shalamwana alisema kwa sasa mradi huo uko katika hatua ya nne ambayo ni usambazaji wa maji katika vituo vikuu.
Afisa Mtendaji wa Kata hiyo Mosses Nkinda alisema mradi huo utaongeza upatikanaji wa maji kwa wakazi hao na kuongeza kasi ya maendeleo na kukuza hali ya kiuchumi mara utakapokamilika.
Kwa upande wake, Mkuu wa wilaya hiyo Moshi Mussa Chang’a alipongeza utekelezaji wa mradi huo na kuwataka viongozi wa kata hiyo kuhakikisha kuwa unakamilika haraka ili wakazi hao waanze kunufaika nao kama ilivyokusudiwa.

0 comments: